Swali
Inafaa Kusikiliza Nasheed na Kaswida zenye Muziki na Vinanda
Jibu
Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu hukumu ya muziki inayotiwa katika Nashiyd na Qaswiydah.
Muziki na utumiaji wa ala za muziki ni haramu katika Dini yetu hii, Uislamu. Zifuatazo ni dalili kuhusu hilo:
Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Kutakuwa watu katika Ummah wangu watakao halalisha uzinzi, uvaaji wa Hariri, pombe (unywaji) na ma’aazif (ala za muziki)” (al-Bukhaariy).
Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Mwisho wa zama (dunia) kutakuwa na maporomoko ya ardhi, mawe kutoka mbinguni na kugeuza kwa wanyama, wakati ambapo ala za muziki na waimbaji wanawake watakapoenea na pombe kuruhusiwa” (atw-Twabaraniy).
Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Watu katika ummah wangu watakunywa pombe, kuiita kwa jina jingine. Watatiwa furaha kwa uchezaji wa ala za muziki na uimbaji wa wanawake (watakao waimbia). Allaah Ataifanya ardhi kuwameza wote na kuwageuza kuwa nyani na nguruwe” (Ibn Maajah).
Na Allaah Aliyetukuka Amesema:
“Na katika watu wako wanaokhitari maneno ya upuuzi ili wawapoteze watu na njia ya Allaah, pasipo wao kujua lolote, na wanaicheza shere hiyo njia ya Allaah. Basi hao watapata adhabu ifedheheshayo” (Luqmaan [31]: 6).
Ibn Jariyr atw-Twabariy katika Jaami‘ul Bayaan amesema kuwa rai ya mufasirina wa Qur-aan kuhusiana na maana ya ibara “Lahwal Hadiyth (maneno ya upuuzi)” inaweza kugawanywa katika aina tatu. Nazo ni:
1. Uimbaji na kusikiliza nyimbo.
2. Kuajiri au kununua waimbaji wataalamu, wanaume na wanawake.
3. Kununua ala za starehe.
Rai hii ndio iliyokuwa rai ya Maswahaba wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama Ibn Mas‘ud, Jaabir bin ‘Abdillaah na Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhum) {al-Kanadi Mustafa Abu Bilaal, The Islamic Ruling on Music and Singing in the Light of the Qur’an, Sunnah and the Consensus of the Salaf (Hukumu ya Kiislamu ya Muziki na Nyimbo katika Muono wa Qur-aan, Sunnah na Ijmaa ya Watangu Wema, uk. 9}.
Na pale Ibn Mas‘ud (Radhiya Allaahu ‘anhu) alipoulizwa kuhusu Aayah hii, alijibu: “Naapa kwa Yule ambaye hakuna Mola ila Yeye kuwa Aayah hii inamaanisha muziki”. Naye aliikariri ibara hiyo mara tatu kuitilia mkazo rai yake hiyo. Na waliokuwa na rai hiyo katika Tabi‘iyn ni ‘Ikrimah, Mujaahid, Makhuul, ‘Umar bin Shu‘ayb na wengineo.
Hata hivyo, upo wakati ambao mashairi yanaruhusiwa kuimbwa bila ya kuwepo kwa ala za muziki isipokuwa daff (dufu, twari) tu kwa wanawake. Na hali hizo ni kama:
1. Wakati wa Jihaad na mapambano mengine katika Njia ya Allaah Aliyetukuka. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiimba wakati wa Vita vya Khandaq (Muslim).
2. Wakati wa sherehe za Kiislamu kama ‘Iyd al-Fitwr na ‘Iyd Al-Adhwhaa.
3. Pia ruhusa imetolewa kwa wanawake na wasichana kuimba na kupiga daff (dufu) wakati wa harusi.
Na Allaah anajua zaidi
Maoni