Madhara Ya Ghiybah - Sababu Za Kutendeka Uovu Wa Ghiybah
1-Kuambatana na marafiki waovu
Moja ya sababu inayosababisha kutenda maasi ya Ghiyba ni kuambatana na marafiki waovu wasiomkhofu Mola wao kwani rafiki muovu humuathiri mwenziwe kwa yale anayoyatenda. Mfano mzuri ametupigia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)
عن أبي موسى الأشعري رضي الله عنه أن النبي صلى الله عليه وسلم قال: (( إنما مثل الجليس الصالح و جليس السوء كحامل المسك ونافخ الكير، فحامل المسك إما أن يحذيك وإما أن تبتاع منه، وإما أن تجد منه ريحاً طيبة، ونافخ الكير إما أن يحرق ثيابك وإما أن تجد منه ريحاًخبيثة)) متفق عليه
Abu Muusa Al-Ash'ariyy (Radhiya Allaahu 'anhu) amesimulia: Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Mfano wa jaliys [mtu unayeambatana naye] mwema na jaliys mbaya ni kamamfano wa mbebaji miski na mfua chuma (anayevuvia kipulizo). Mbebaji miski ima atakupa au utanunua kutoka kwake au utapata harufu nzuri kwake. Na mfua chuma (anayepuliza kipulizo), ima atachoma nguo zako au utapata harufu mbaya kutoka kwake)) [Al-Bukhaariy na Muslim]
2-Kutokuzingatia aibu zake mwenyewe kwanza
Ghiybah ni maovu yanayopatikana katika kila jamii takriban. Hakika ni maradhi maovu kabisa yanayoleta madhara makubwa baina ya ndugu wa Kiislamu kwa kukashifiana na kutangaziana aibu zao. Tutambue kuwa hakuna binaadamu aliyekamilika, na kila mtu atakuwa na aibu zake kama si yeye mwenyewe binafsi basi ni katika familia yake, na kama si familia yake basi ni wa karibu yake n.k. Hata kama hakuna aibu yoyote kwake au kwa watu wake, basi akhofu kuwa huenda ikamfikia yeye aibu hiyo au ndugu zake au watoto wake au yeyote katika jamaa zake, hii imedhihirika sana kuwa ni malipo yanayowapata wanaopenda kusengenya wenzao, Allaah Huwalipa watu wa aina hiyo hapa hapa duniani kwa kuwafika aibu na mengineyo.
3-Simu ni chanzo kikuu
Chanzo kikuu kinachofanikisha kutendeke Ghiybah na uzushi kuenea katika jamii kwa siku hizi, hasa katika nchi zilizoendelea ambako uchumi wao uko juu na gharama za mawasiliano ni rahisi mno na pia kuweko simu za bure ambazo kwa wengine huwa ndio kama chakula chao; huamka asubuhi na kitu cha kwanza ni kutafuta uzushi, umbeya na usengenyaji kwa mzushi kama yeye na kuanza kutangaza. Lau kama simu zingelikuwa ni za kulipiwa basi bila shaka wangelifilisika wenye kupenda kusengenya na kuzusha. Ama nchi nyingine ambako simu hulipiwa, pia nako uzushi unaenea kutokana na wepesi wa mawasiliano baina ya jamaa katika mikusanyiko mbali mbali ya kutembeleana au ya kishuguhuli za jamii na vikao vya mabarazani.
4-Kudhani kwamba kusikiliza tu hakuhusu kusengenya
Mara nyingi utamsikia mtu anasema: "Lakini mimi nasikiliza tu umbeya sitii langu". Mwenye kusema hivi atambue kuwa mwenye kusengenya na mwenye kusikia wote wako katika ushirikiano wa maovu haya. Na kila kiungo cha binaadamu kitamchongea mwenye kufanya maasi siku ya Qiyaamah, hivyo masikio yatakuchongea unaposikiliza umbeya au usengenyaji kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema:
((إِنَّ السَّمْعَ وَالْبَصَرَ وَالْفُؤَادَ كُلُّ أُولئِكَ كَانَ عَنْهُ مَسْؤُولاً))
((Hakika masikio, na macho, na moyo hivyo vyote vitaulizwa)) [Al-Israa: 36]
5-Kujishughulisha na upuuzi badala ya kutumia muda kwa manufaa
Muda ni neema ambayo inampasa Muislamu ashukuru; amejaaliwa kuwa yuhai, kwani kila dakika ni muhimu kuitumia ipasavyo kwa kujichumia mema na sio kuipoteza kwa mambo ya upuuzi khaswa yanayoweza kumuamgamiza mtu motoni kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((فَوَيْلٌ يَوْمَئِذٍ لِلْمُكَذِّبِينَ))
(( الَّذِينَ هُمْ فِي خَوْضٍ يَلْعَبُونَ))
((Basi ole wao siku hiyo hao wanaokadhibisha))
((Ambao wanacheza katika mambo ya upuuzi)) [At-Twuur: 11-12]
Amesema Imaam Ibn Kathiyr: "Ni wale ambao duniani wanacheza katika mambo ya batili" Na kusengenya ni maovu, dhambi na batili inayompasa Muislamu ajiepushe nayo.
Inaendelea
Maoni