Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Swalah ya Eid

Hukumu ya swalah ya ´Iyd

Ndugu muislamu! Jifunze baadhi ya hukumu muhimu unazotakiwa kuzijua zinazohusiana na mwezi huu mtukufu.

Swalah ya ´Iyd

Kwa mujibu wa wanachuoni wengi swalah ya ´Iyd ni faradhi kwa baadhi ya waislamu. Inajuzu kwa baadhi kutoiswali. Hata hivyo imependekezwa kuihudhuria na mtu kushirikiana na ndugu zake waislamu. Ni Sunnah iliyokokotezwa isiyotakikana kuachwa isipokuwa kwa kuwepo udhuru wa Kishari´ah.

Baadhi ya wanachuoni wanaonelea kuwa ni lazima kwa waislamu wote kuiswali kama swalah ya Ijumaa. Wanaume wote katika mji na ambao wana majukumu juu ya matendo yao ni lazima waiswali. Maoni haya ndio yanaonekana kuwa dalili yenye nguvu na ilio karibu zaidi na usawa.

Ni Sunnah kwa wanawake kuihudhuria. Lakini wanatakiwa kuzingatia kujisitiri vizuri na kutojitia manukato. Imethibiti kwa al-Bukhaariy na Muslim ya kwamba Umm ´Atwiyyah (Radhiya Allaahu ´anhaa) amesema:

“Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) ametuamrisha kuwatoa nje siku ya ´Iyd mbili wanawake vijana ambao ndio karibuni wametoka kukomaa, wanawake wenye hedhi na mabikira. Kuhusiana na wanawake wenye hedhi, wajitenge mbali na kuswali.”[1]

Katika upokezi mwingine imekuja:

“Ee Mtume wa Allaah! Mmoja wetu hana Jilbaab ya kutoka nayo?” Akasema: “Dada yake ampe moja katika Jilbaab zake.””[2]

Ni jambo lisilo na shaka ya kwamba haya yanafahamisha kuwa imekokotezwa kwa wanawake kutoka na kuswali swalah za ´Iyd na washiriki kheri na du´aa ya waislamu.

Lililo Sunnah kwa anayefika mahala pa kuswalia swalah ya ´Iyd au swalah ya mvua akae moja kwa moja na wala asiswali Rakaa´ mbili za Sunnah kwanza. Kutokana na ninavyojua kitu kama hicho hakikupokelewa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) wala Maswahabah zake (Radhiya Allaahu ´anhum). Isipokuwa tu ikiwa inaswaliwa msikitini. Katika hali hii atatakiwa kuswali Rakaa´ mbili za Sunnah kutokana na jumla ya maneno yake Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam):

“Mmoja wenu atapoingia msikitini asikae mpaka kwanza aswali Rakaa´ mbili.”[3]

Kwa ambaye amekaa na kusubiri swalah ya ´Iyd imewekwa katika Shari´ah akithirishe kusema “Laa ilaaha illa Allaah” na “Allaahu Akbar”. Ni nembo ya siku hiyo. Ni Sunnah kwa wote waliyoko ndani ya msikiti na nje ya msikiti mpaka Khutbah itapoisha. Ni sawa vilevile kujishughulisha na kusoma Qur-aan.

Napendelea kuweka wazi kwamba asli Takbiyr inatakiwa kutamkwa usiku wa ´Iyd na kabla ya swalah ya ´Iyd pamoja vilevile na yale masiku kumi ya mwanzo ya Dhul-Hijjah na masiku ya Tashriyq. Imewekwa katika Shari´ah kwenye masiku haya matukufu. Ndani yake mna fadhila tele kutokana na maneno ya Allaah (Ta´ala) juu ya Takbiyr katika mnasaba wa ´Iyd baada ya Ramadhaan:

وَلِتُكْمِلُوا الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُوا اللَّـهَ عَلَىٰ مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ

“… na ili mkamilishe idadi na ili mumkabiri Allaah kwa kuwa amekuongozeni na mpate kushukuru.”[4]

Allaah (Ta´ala) amesema pia kuhusu yale masiku kumi ya mwanzo ya Dhul-Hijjah na masiku ya Tashriyq:

لِّيَشْهَدُوا مَنَافِعَ لَهُمْ وَيَذْكُرُوا اسْمَ اللَّـهِ فِي أَيَّامٍ مَّعْلُومَاتٍ عَلَىٰ مَا رَزَقَهُم مِّن بَهِيمَةِ الْأَنْعَامِ ۖ فَكُلُوا مِنْهَا وَأَطْعِمُوا الْبَائِسَ الْفَقِيرَ

“… ili washuhudie manufaa yao na walitaje Jina la Allaah katika siku maalumu kwa yale aliyowaruzuku kati ya wanyama wenye miguu minne wa mifugo. Basi kuleni humo na lisheni mwenye shida fakiri.”[5]

Allaah (´Azza wa Jall) amesema vilevile:

وَاذْكُرُوا اللَّـهَ فِي أَيَّامٍ مَّعْدُودَاتٍ

“Mdhukuruni Allaah katika siku za kuhesabika.”[6]

Katika masiku haya maalum na yaliyotengwa imewekwa katika Shari´ah kumdhukuru Allaah kwa Takbiyr ambazo hazikufungamana na zilizofungamana. Ni jambo lina asli katika Sunnah twaharifu na matendo ya Salaf. Njia ya Takbiyr iliyowekwa katika Shari´ah ni kila muislamu kusema “Allaahu Akbar” kivyake. Anatakiwa kunyanyua sauti yake kiasi cha kwamba wengine waweze kumsikia ili wamuige na wadhukuru kupitia yeye. Kuhusu Takbiyr za kwa pamoja na zilizozuliwa, ni watu wasiopungua wawili wanyanyue sauti zao za Takbiyr kwa njia ya kwamba wanaanza na kumaliza kwa pamoja na wanafanya hivo kwa sauti ya pamoja na kwa njia maalum. Kitendo hichi hakina asli wala hakina dalili. Ni uzushi. Allaah hakuteremsha dalili yoyote juu ya hilo.

´Iyd ikiangukia siku ya Ijumaa ambaye ameswali swalah ya ´Iyd ana khiyari ya kuswali swalah ya Ijumaa au Dhuhr. Imethibiti kuwa Mtume (Swalla Allaahu ´alayhi wa sallam) amesema:

“Leo zimekutana sikukuu mbili. Aliyeswali ´Iyd hahitajii kuswali Ijumaa.”[7]

Lakini hatakiwi kuacha kuswali Dhuhr. Lililo bora ni yeye kuswali swalah ya Ijumaa pamoja na wengine. Iwapo hatoswali swalah ya Ijumaa anatakiwa badala yake kuswali Dhuhr.

Kuhusu imamu anatakiwa kuswali swalah ya Ijumaa pamoja na wale waliohudhuria wakiwa hawapungui watu watatu pamoja na imamu. Endapo hakutohudhuria isipokuwa mtu mmoja tu ataswali Dhuhr pamoja naye.

Ni sawa kwa muislamu kumwambia ndugu yake siku ya ´Iyd au siku nyengine:

“Allaah atukubalie sisi na nyinyi matendo yetu mema.”

[1] al-Bukhaariy (324) na Muslim (890).

[2] Muslim (890).

[3] al-Bukhaariy (1167) na Muslim (714).

[4] 02:185

[5] 22:28

[6] 02:203

[7] Abu Daawuud (1073) na Ibn Maajah (1311). Swahiyh kwa mujibu wa al-Albaaniy katika ”Swahiyh Abiy Daawuud” (948).

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Hukumu ya kupeleka barua ya posa kwenye kitambaa cheupe

                      Hukumu ya kupeleka barua ya posa kwenye kitambaa cheupe  Hakika ni kuwa posa ilivyofanyika katika Uislamu kuanzia wakati wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) inafahamika vilivyo. Posa inaweza kuja kutoka kwa mume na watu wake kwa jamaa za mke au mzazi wa mke kumtafutia binti yake mume. Ikiwa wazazi watakwenda kwa wazazi wa mke, baada ya kupeleka maneno, na wazazi wa mke watataka kupatiwa muda wa kufikiria, kufanya shuuraa, kuulizia, kutafiti na baadaye kukubali au kukataa. Ikiwa wamekubali baada ya kumshauri binti  yao  ni vyema mume mtarajiwa aende amuone atakaye kuwa mkewe ili apate kutulia na kuridhika kabla siku ya Nikaah. Binti huyo au wazazi wake wataweka kiwango cha mahari ambacho mume anatakiwa kutoa. Hii njia ya kuweka pesa kwenye kitambaa au bahasha haipo katika mafunzo ya Kiislam, na huenda ni njia ya kitamaduni fulani au itikadi f...

Maana ya Uadilifu

                                         MAANA  YA  UADILIFU  KATIKA  UISLAMU Assallaam  Aleykum  WarahmatulLaah  Wabarakatuh Alhamdu Lillaahi Rabil'aalamiyn) Allaahumma Swalli 'alaa Muhammad wa 'alaa aali Muhammad kamaa Swallayta 'alaa Ibraahiym wa 'alaa aali Ibraahiym wa Baarik 'alaa Muhammad wa 'alaa aali Muhammad kamaa Baarakta 'alaa Ibraahiym wa 'alaa aali Ibraahiym fil'aalamyna Innaka Hamiydun Majiyd. Ndugu zangu Waislam Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema katika Qur-aan. إِنَّ اللَّـهَ يَأْمُرُ بِالْعَدْلِ وَالْإِحْسَانِ وَإِيتَاءِ ذِي الْقُرْبَىٰ وَيَنْهَىٰ عَنِ الْفَحْشَاءِ وَالْمُنكَرِ وَالْبَغْيِ ۚيَعِظُكُمْ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ Hakika Allaah Anaamrishia uadilifu na ihsaan na kuwapa (mahitajio na msaada) jamaa wa karibu; na Anakataza machafu na munkari na ukandamizaji. Anakuwaidhini huenda mkapata kukumb...

Viungo vya Mwili vitashuhudia Matendo ya Mwanaadamu Siku ya Qiyaamah

Anasema Allaah  سبحانه وتعالى   ((الْيَوْمَ نَخْتِمُ عَلَى أَفْوَاهِهِمْ وَتُكَلِّمُنَا أَيْدِيهِمْ وَتَشْهَدُ أَرْجُلُهُمْ بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ)) ((Leo Tunaviziba vinywa vyao, na iseme Nasi mikono  yao , na itoe ushahidi miguu  yao kwa waliyokuwa wakiyachuma))  [Yaasiyn :65 ] Siku ya Qiyaamah viungo vya miili vitakuwa ni vyenye kushuhudia matendo ya binaadamu aliyoyatenda hapa duniani: Mfano mikono itasema: "nimeiba".  Miguu itasema, "nimekwenda sehemu ya ma'asi". Macho yatasema, "nimetazama machafu".  Masikio yatasema, "nimesikiliza nyimbo, au umbea" na kadhalika. Na hivi ndivyo itakavyokuwa hali ya makafiri, wanafiki na wenye kumuasi Mola siku ya kufufuliwa,  watakapokanusha madhambi waliyoyatenda duniani na kuapa kwamba hawakuyafanya, Allaah  سبحانه وتعالى  Atawafunga midomo  yao na kuviamrisha viungo vizungumze:   عن أنس بن مالك قال: كنا عند النبي صلى ال...